MTOTO AFA KWA KUNG`ATWA NA FISI

Kamanda wa Polisi Mkoani Shinyanga, Evarist Mangalla
Mtoto Joha Shija (3), mkazi wa kijiji cha Ngulu katika kata ya Ngogwa wilayani Kahama mkoani Shinyanga, amefariki dunia baada ya kung’atwa na  fisi aliyevamia nyumbani kwao usiku kwa lengo la kushambulia mifugo na kuwajeruhiwa watu wengine watatu wakiwemo wazazi wake.

Tukio hilo lilitokea Machi 21, mwaka huu saa 8:00 usiku na fisi huyo kumshambulia kwa kumng’ata mtoto huyo sehemu za usoni, puani, mdomoni na kumnyofoa macho na kufariki dunia muda mfupi.

Kamanda wa Polisi Mkoani Shinyanga, Evarist Mangalla, alisema jana kuwa chanzo cha tukio hilo ni fisi huyo kuvamia zizi la mifugo lililopo kando ya nyumba wanayoishi na kutaka kushambulia mifugo.

Alisema baada ya baba wa marehemu, Shija Masolwa, kusikia kelele za mifugo alitoka nje ya nyumba walimokuwa wamelala  kwa lengo la kupambana na fisi huyo akisaidiwa wa mdogo wake, Maneno Masolwa, lakini walizidiwa nguvu na kulazimika kukimbilia ndani huku wakifuatwa na mnyama huyo.

Kwa mujibu wa Kamanda Mangalla,  baada ya fisi kuingia ndani alimshambulia mtoto huyo aliyekuwa amelala huku Shija akijeruhiwa kwa kung’atwa na kunyofolewa kidole gumba cha mkono wa
kushoto na goti la kushoto.

Maneno Masokwa alijeruhiwa kwa kung’atwa tako la kulia huku Ngema Shija akijeruhiwa kwa  kung’atwa kwenye goti.
Wote walitibiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama na kuruhusiwa baada ya hali zao kuwa nzuri.

Comments