Polisi Ruvuma wawasaka waliomuua mwenzao

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma, Deusdedit Nsimeki
Jeshi la Polisi mkoani Ruvuma limeimarisha ulinzi kwa kupeleka askari polisi kwenye maeneo mbali ya wilaya ya Namtumbo, baada ya kutokea mauaji ya raia mmoja na askari polisi wilayani humo.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma, Deusdedit Nsimeki, askari polisi huyo aliuawa na wananchi wa kijiji cha Ngwinde wilayani Namtumbo baada ya kudaiwa kumfyatulia risasi mwendesha piki piki Makisio Ngonyani na kumsababishia kifo.

 Alisema katika hatua ya awali, jeshi la polisi limeweka mkakati wa kuwakamata watuhuhumiwa wote wa tukio hilo na kwamba upelelezi umekwishaanza.

Alisema katika tukio hilo, askari mmoja alijeruhiwa na amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Ruvuma mjini Songea.

 Kamanda Nsimeki alisema hali ya askari huyo, PC Kamugisha, inaendelea vizuri na anaendelea kupatiwa matibabu hospitalini hapo.

 Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Ruvuma ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa huo, Said Mwambungu, alisema ameviagiza vyombo vya ulinzi na usalama mkoani humo kuhakikisha kuwa wahusika wa matukio hayo wanakamatwa mara moja na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Tukio hilo lilitokea Machi 23 mwaka huu majira ya saa 8 mchana katika ya vijiji vya Litola na Ngwinde wilayani Namtumbo

Comments