STORI YA MWANAFUNZI WA IFM ALIYRKUTWA AMEKUFA HOSTEL

Chuo cha IFM
Mwanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), Ibrahim Jackson (24), amekutwa akiwa amekufa katika chumba cha kupumzikia kilichopo chuoni hapo bila mwili wake kuwa na jeraha lolote.
 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Marietha Minangi, alisema tukio hilo lilitokea saa 11:30 juzi jioni katika chumba namba 118 jengo namba D kilichopo mtaa wa Shaban Robert.
 
Jamiileotz lilifika IFM na kuzungumza na Mshauri wa Wanafunzi, Emmanuel Mushi, ambaye alisema kuwa marehemu alikuwa anasomea Shahada ya Usimamizi wa Kodi akiwa mwaka wa pili.
 
Alisema marehemu alikuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa kifafa kwa muda mrefu kabla hata hajajiunga na IFM.
 
Alisema juzi jioni marehemu aliomba funguo kwa ajili ya kwenda kupumzika katika chumba kinachotumiwa kulala na wanafunzi kutoka nje ya nchi pindi wanapofika chuoni hapo  kwa ajili ya masomo.
 
“Nyaraka zake zinaonyesha marehemu alikuwa anasumbuliwa na ugonjwa wa kifafa kwa muda mrefu, hata kabla hajajiunga na chuo hiki, kwa hapa chuoni ugonjwa huo ulikuwa unamtokea mara kwa mara,” alisema Mushi.
 
Aliongeza kuwa mara baada ya kupewa funguo alikwenda kupumzika katika chumba hicho na baadaye alikutwa amefariki huku mwili wake ukiwa umelala kitandani.
 
Alisema baada ya tukio hilo walitoa taarifa katika kituo cha polisi na polisi walifika katika chumba hicho na kumpeleka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa uchunguzi zaidi.
 
Mushi alisema wamewasiliana na wazazi wake waliopo wilaya ya Mbozi Mkoani Mbeya na taratibu za kuusafirisha mwili huo zitafanyika leo.
 
Mmoja wa marafiki wa karibu wa  marehemu, Peter Alphonce, aliliambia jamiileotz kuwa alikuwa na marehemu siku moja kabla ya kifo chake wakicheza mpira na walimaliza kucheza vizuri na kuagana kuelekea hosteli.
 
“Nilikuwa naye jana (juzi) tukicheza mpira, hadi saa kumi tulipomaliza aliniaga na kuelekea katika Machava Hostel ndiko anakolala,” alisema Alphonce.

Comments