Waasi Wadaiwa Kuipinduwa Serikali Jamhuri ya Kati

Waasi Wadaiwa Kuipinduwa Serikali Jamhuri ya Kati
WAASI wanadaiwa kuipindua serikali ya Rais Francois Bozize wa Jamhuri ya Kati, wamesema kwamba watasimamia serikali ya umoja wa kitaifa iliyopo, ikiwa na marekebisho madogo
.
Huku Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini akisema wanajeshi 13 wa nchi yake wameuwawa katika mapigano nchini Afrika ya Kati walikokuwa wakipigana dhidi ya waasi. Taarifa hizo ni kwa mujibu wa msemaji kutoka upande wa wapiganaji hao baada ya kiongozi wa Seleka, Michel Djotodia, kumuondoa Francois Bozize hapo jana.
Akizungumza na Shirika la habari la Reuters kwa njia ya simu, msemaji huyo Eric Massi amesema waziri mkuu wa sasa ataendelea kubakia madarakani na baraza la mawaziri litafanyiwa mabadiliko kidogo.
Akizungumzia hali ilivyo sasa katika maeneo ya mji mkuu wa Jamhuri ya Afrika Kati, Bangui na alijagamba kwamba mji huo kwa sasa upo katika udhibiti wao na upo tulivu, ingawa aliongeza kuwa wanahitaji kufanya jitihada zaidi katika suala la usalama katika viunga vya jiji hilo kwa lengo la kukomesha kabisa vitendo vya uporaji.
Kwa upande wake Mjumbe wa Umoja wa Mataifa anayeshughulia masuala ya haki za binadamu akiwa Bangui, Amy Martine amesema “Tuna wasiwasi, umeme umekatwa katika mji wa Bangui,kwa hivyo Bangui hakuna umeme kama ilivyokuwa jana. Mchana huu maji yamekatwa. Kwa hivyo hali hii itakuwa maskikitiko makubwa kwa watu wa Bangui na tatizo endapo tatizo hilo halijatatuliwa katika siku zijazo”
Katika duru nyingine, Rais Jacob Zuma amesema wanajeshi 13 wa Afrika Kusini walikuwemo nchini humo wameuwawa katika mapigano makali yaliyotokea mwishoni mwa juma na wapiganaji waasi ambao kwa hivi sasa wanaushikilia mji wa Bangui.
Akizungumza katika mkutano wake na waandishi habari rais Zuma amesema wanajeshi wengine 27 wamejeruhiwa huku kukiwa na idadi nyingine ya askari ambayo haijulikani ilipo. Akieleza kusikitishwa kwake na mkasa huo rais Zuma amesema ni wakati wa kuhuzunisha kwa taifa hilo.
Januari mwaka huu Afrika Kusini iliepeleka askari 200 huko Jamhuri ya Afrika Kati kwa ajili ya kutoa mafunzo ya kijeshi kwa askari wa taifa hilo ikiwa ni shabaha ya kuliwezesha kukabiliano na muungano wa waasi wa Seleka, kulikotokana na uvamizi wao walianza kuufanya mapema Desemba mwaka jana.
Baada ya wa makubaliano ya mpango wa amani wa Januari, uliyosainiwa huko mjini Libraville nchini Gabon, wenye shabaha ya kuunda serikali ya mgawanyo wa madaraka, kiongozi wa waas Djotodia alitajwa kuwa naibu waziri mkuu. Makubaliano hayo yalitaka mgawanyo wa madaraka ufanyike kwa kuhusisha waasi,upinzani pamoja na utawala wa Bozize.
Waasi wanamtuhumu Bozize kwa kukiuka makubaliano na kufanya waanzishe tena vita Alhamisi iliyopita. Operesheni yao ilikwenda kwa kasi na kudhibiti kwa haraka eneo la kusini mwa mji wa Bangui, wenye utajiri mkubwa madini katika taifa hilo lililokuwa koloni la Ufaransa.

Comments