Hatimaye harufu ya ufisadi yabainika kuingia katika halmashauri za jiji laTanga

Kamati  ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa(LAAC) imeagiza kuchukuliwa hatua kali  na kusimamishwa kazi Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Korogwe, Sadiki Kallaghe, kwa tuhuma za kusaini mkataba  wa kumpa tenda ya kukusanya ushuru wa halmashauri  mzabuni bila kumshirikisha mwanasheria wala mkurugenzi wa halmashauri hiyo.

Agizo hilo limetolewa na Mwenyekiti wa LAAC, Rajabu Mbarok, katika majumuisho ya ziara yao katika ofisi za mkuu wa mkoa  wa Tanga na kushirikisha wakuu wa idara, wakurugenzi, wenyeviti wa halmashauri, mkuu wa mkoa na wakuu wa wilaya.Mbarok  alimuagiza Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Bendkito Ole Kuyani, kuunda kamati ya kuchunguza suala hilo huku akitaka mwenyekiti huyo asimamishwe kazi ili kuepuka kuharibu uchunguzi. Mbarok alisema wametembelea miradi sita katika halmashauri hiyo ikiwamo soko la kimataifa linalojengwa maeneo ya Makuyuni na kwamba miradi hiyo hairidhishi na kutolea mfano choo kilichojengwa kwa thamani ya Sh. milioni saba ambacho hakilingani na thamani halisi ya fedha.

Alisema halmashauri ya Korogwe imekuwa ikipata hati chafu kwa muda wa miaka mitano sasa na zaidi ya Sh. bilioni moja hazikutumika.Kuhusu halmashauri ya Mji Mdogo wa Korogwe, alisema walikagua miradi mitano, lakini miradi yenye nafuu ni miwili tu hiyo mingine ipo chini ya viwango huku akimpa onyo mkurugenzi wa mji wa Korogwe kwa kuikimbia kamati hiyo na kwenda kujificha na kuwa wamekaidi agizo la  mkuu wa wilaya na mkuu wa mkoa hawawapandishi vyeo walimu na kuwaongezea mishahara mpaka sasa.

Katika Jiji la Tanga alisema walikagua mradi wa bwawa la umwagiliaji liliyopo Mabaayani lakini aligundua ufisadi mkubwa na kusema kuwa mradi huo ni wa watendaji na sio wananchi kwani mpaka sasa zaidi ya MSh. mlioni 300katika mradi huo zimeliwa na wajanja.

Comments