JAMAA AHUKUMIWA KIFUNGO MIAKA 65 JELA KWA KUMPA UJAUZITO MTOTO WAKE WA KUMZAA HUKO MBEYA





MKAZI wa Mtaa wa Uhamila katika mji mdogo wa Rujewa, mkoani Mbeya, amehukumiwa miaka 65 jela kutokana na makosa matatu tofauti, yaliyotokana na kumpa ujauzito mwanawe wa kumzaa.    Mahakama ya Wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya ilitoa hukumu hiyo jana kwa Benjamin Muyinga (48) baada ya kutiwa hatiani kwa makosa hayo.


Hakimu Mfawidhi Kinabo Minja alimhukumu mshitakiwa kutumikia jela miaka 30 kwa kosa la kufanya mapenzi na mtoto wake, miaka 30 mingine kwa kubaka mtoto wake na miaka mitano jela kwa kumpa mimba mwanafunzi.

Minja alisema ameridhishwa na ushahidi uliotolewa mahakamani hapo hivyo atatumikia adhabu hiyo kwa pamoja kwa maana kwamba atakaa jela miaka 30.

Mashitaka yaliyokuwa yakimkabili mahakamani hapo ni kufanya mapenzi na mtoto wake, kubaka mtoto wake na la tatu ni kumpa mimba mwanafunzi.

Awali ilidaiwa mahakamani na Mwendesha Mashitaka wa jeshi la Polisi, Mazoya Luchagula, mbele ya Hakimu Mfawidhi Kinabo Minja, Oktoba 18 mwaka jana, mwanafunzi (jina linahifadhiwa) aliyekuwa na umri wa miaka 14, alikuwa mjamzito.

Luchagula alidai walimu wa shule hiyo ndiyo walitilia shaka suala la mwanafunzi huyo aliyekuwa darasa la tano katika shule ya msingi iliyoko Rujewa kwamba alikuwa na ujauzito. Alipelekwa hospitali na kwenda kukutwa akiwa na mimba ya miezi minne.

Kwa mujibu wa Mwendesha Mashitaka, baada ya kuhojiwa, mwanafunzi huyo alidai ujauzito ulikuwa wa baba yake mzazi waliyekuwa wakiishi naye wawili nyumbani kutokana na baba yake kutengana na aliyekuwa mkewe ambaye hivi sasa anaishi jijini Mbeya.

Mwanafunzi huyo alibainisha namna alivyokuwa akiishi na baba yake baada ya wazazi wake kutengana na kwamba alimgeuza ‘mkewe’ kwani alikuwa akilala naye na kufanya naye mapenzi hadi ilipobainika kuwa na ujauzito huo.

Katika kile kilichoelezwa na upande wa mashitaka kwamba kitendo kilichofanywa na mzazi huyo hakikubaliki katika jamii ya Watanzania, Mwendesha Mashitaka aliomba mahakama kutoa adhabu kali kwa mshitakiwa iwe fundisho kwake na wazazi wengine wenye tamaa zenye kusababisha ukatili dhidi ya watoto wao.

Comments