Abiria wa treni 1,200 wakwama

Waziri wa uchukuzi, Harrison Mwakyembe.
Abiria zaidi ya 1,210 wamekwama mkoani hapa kutokana na njia ya reli kuharibika maeneo ya Gulwe na Godegode wilayani Mpwapwa.
 
Abiria hao ambao walikuwa wakitokea Kigoma kuelekea Dar es Salaam walifikia mkoani hapa jana saa 5:30 asubuhi jana baada ya kuondoka Kigoma Jumapili.
 
Jamiileotz ilishuhudia abiria hao wakiwa katika kituo cha stesheni ya Dodoma wakirandaranda huku wengine wakitafuta magari kwa ajili ya kuendelea na safari.
 
Baadhi yao walisema safari yao ilikuwa na mashaka kutokana na injini ya treni hiyo kuharibika.
 
Issa Kikolwa alisema: “Leo ni siku ya tatu mpaka sasa tupo Dodoma wakati tumezoea siku kama ya leo tunakuwa Dar es Salaam…na hapa tulipo hatujui tutafika lini kwa hali ilivyo”
 
 “Tumeambiwa kuwa tunaweza kuondoka muda ya saa moja…kama hali itakuwa nzuri, lakini hatuna uhakika na hilo…ila muda mfupi tumetangaziwa kuwa tuje tujipange kwenye dirisha la kukatia tiketi tukiwa na tiketi na vitambulisho vyetu na hatujui wanataka kutuambia nini,” alisema.
 
Hassan Ayoub, alisema tatizo lilianza kuonekana juzi kati ya maeneo ya Tabora na Igoma baada ya injini za treni kuzima.
 
“Ilibidi tulale maeneo hayo kuanzia saa saba usiku hadi saa 11 alfajili na kuanza safari hadi kufika hapa, pia tumeambiwa hatuwezi kuendelea na safari kutokana na reli kujaa maji,” alisema.
 
Alisema kutokana na hali hiyo, wamejikuta wakimaliza fedha za kujikimu njiani huku wakilipia huduma za choo na kununua maji. 
 
Saada Ferouz alisema wamepata matatizo makubwa wakiwa njiani kwani walifika eneo la Isinge treni hiyo iliharibika ikawalazimu kulala eneo hilo.
 
Mkuu wa Kituo cha Kampuni ya Reli Tanzania (TRL) cha Dodoma, Selsus Roman, aalithibitisha kutokea kwa tatizo hilo na kudai kuwa abiria hao walitarajia kuondoka jana jioni iwapo eneo hilo litatengamaa.
 
Alisema abiria hao waliingia jana saa 5:30 asubuhi wakitokea Kigoma na kuwa walishindwa kuendelea na safari kutokana na maji kujaa kwenye eneo la Gulwe na Godegode.
 
“Mvua zilinyesha sana kuanzia Jumapili hadi juzi usiku na eneo hilo limejaa maji kwa hiyo mafundi wapo huko kwa ajili ya kufanya matengenezo, hivyo yakikamilika abiria wataendelea na safari leo (jana) jioni,” alisema.
 
Roman alisema walipeleka taarifa makao makuu kutokana na suala hilo na kutakiwa kuwasaidia posho kwa ajili ya chakula ambayo ni Sh. 2,500 kwa kila mmoja.
“Tumewaambia wapange fedha za kujikimu na tumemtaka kila abiria alete tiketi na kitambulisho chake ndiyo tuwape fedha za kujikimu,” alisema.

Comments

Popular Posts