Bilal ataka wezi wa maji washughulikiwe

Makamu wa Rais, Dk. Mohammed Gharib Bilal
Makamu wa Rais, Dk. Mohammed Gharib Bilal, amewataka watu wote wanaojiunganishia maji kwa njia za wizi na kuwasababishia wengine kukosa huduma hiyo ya msingi na serikali kupata hasara, kudhibitiwa.
 
Dk. Bilal, alitoa agizo hilo jana jijini Dar es Salaam, wakati wa ziara yake katika Mamlaka ya Majisafi na Majitaka jijini humo (Dawasa).
 
 “Ni wajibu wetu kuhakikisha wale wote wanaotumia maji wanatumia kwa njia ya halali. Tujitahidi kuwadhibiti hao wagemaji njiani (wanaojiunganishia maji kwa njia zisizo halali) ili yafike mahali yanakotakiwa kufika,” alisema Dk. Bilal.
 
Alisema ni vizuri kuhakikisha miundombinu ya huduma hiyo inatunzwa na kwamba maji yanayopatikana yanakuwa safi na salama.
 
Pia aliagiza kuharakishwa kwa miradi ya maji ya Kidunda, Mpiji na Mpera kwa kuwa ni ya muhimu.
 
Kwa upande wake, Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe, alimthibitishia Makamu wa Rais, kuwa wizara yake imeshachukua hatua za kufuatilia utekelezaji wa miradi hiyo na kwamba mpaka sasa tayari kiasi cha fedha  kimeshapatikana.
 
Alisema Sh. takribani bilioni 27 zinahitajika hadi kukamilika kwa miradi hiyo mitatu ya maji.
 
 Akizungumzia hali ya  rasilimali ya maji nchini, Profesa Maghembe, alisema kuwa kiasi cha rasilimali kimepungua kutokana na kiwango kidogo cha mvua zilizonyesha kati ya Novemba mwaka jana hadi mwaka huu.
 
Baadhi ya maeneo yaliyoathiriwa na hali hiyo ni mabonde ya maji ya mito Wami/Ruvu,  maziwa ya Tanganyika na Nyasa huku mabonde ya Ziwa Viktoria na Bwawa la Mtera vikibaki katika hali ya kawaida.

Comments

Popular Posts