Hofu ya ufisadi yatanda hospitali ya wilaya Manyoni

Serikali imetakiwa kutuma wachunguzi katika hospitali ya wilaya ya Manyoni mkoani Singida, ili kubaini ubadhirifu wa mabilioni ya fedha zinadaiwa ‘kutafunwa’ na baadhi ya uongozi wa hospitali hiyo.
 
Kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari, ubadhirifu huo ni wa muda mrefu,  jambo linalosababisha hospitali hiyo kukosa hadhi ya ngazi ya wilaya.
 
Taarifa zaidi zinadai kuwa, madaktari na manesi katika hospitali hiyo, wameshakutana mwishoni mwa mwaka uliopita, kujadili changamoto zinazowakabili, ikiwemo upotevu wa fedha zinazotolewa kwa ajili ya uboreshai huduma za afya.
 
Ilidaiwa kuwa ufisadi unaofanyika hospitalini hapo umesababisha upungufu kadhaa ikiwemo ukosefu wa vitendea kazi.
 
Kwa mujibu wa vyanzo vya gazeti hili, kiasi cha Shilingi milioni 26 kutoka serikalini, zinatolewa kila mwezi hospitalini hapo, lakini ‘zinaishia’ mifukoni mwa watumishi wasiokuwa waminifu.
 
Mmoja wa madaktari (jina limehifadhiwa) alisema miongoni mwa vifaa muhimu vinavyokosekana hospitalini hapo ni mashine ya oxygen, hivyo kusababisha wagonjwa wengi wakiwemo watoto wanaozaliwa kabla ya muda wao, kupoteza maisha.
 
Alivitaja vifaa vingine ni vipimo vya shinikizo la damu, joto la mwili na ultrasound, hivyo kusababisha wagonjwa kwenda katika hospitali ya mkoa wa Dodoma.
 
Chanzo chetu kilienza kuwa hospitali hiyo haina daktari bingwa wala utaratibu kupima wagonjwa wodini unaotakiwa kufanywa mara mbili au tatu kwa siku, kulingana na afya ya mgonjwa.
 
Kaimu Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Dk Jackson Kitundu, alithibitisha kuwepo upungufu huo ikiwemo kutokuwepo ultrasound.
 
Pia alisema mashine nyingine kama ya oxgen, wanasubiri mgawo kutoka Bohari Kuu ya Dawa (MSD).
Dk Kitundu alisema madai ya Shilingi milioni 26 zinazodaiwa kufanyiwa ufisadi hospitalini hayana ukweli, kwa vile fedha zinazotambulika ni Shilingi milioni 13.
 
“Inawezekana serikali inatoa fedha hizo kwa kila mwezi, ila mimi nakabidhiwa na mkuu wangu (hakumtaja jina) Shilingi milioni 13 kwa mwezi, fedha ambazo hutumika kulipa madeni mbalimbali,” alisema

Comments

Popular Posts