Mawaziri waeleza shule wanazosoma watoto wa
Waziri wa Nchi Ofisi ya rais Mahusiano na Uratibu, Stephen Wasira
Miongoni mwa waliozungumza na NIPASHE kwa njia ya simu, wameeleza
kwamba watoto wao wanasoma hapa nchini kwenye shule za serikali japokuwa
kuna taarifa kwamba watoto wao wanasoma nje ya nchi na kwenye shule
binafsi za gharama hapa nchini.
Baadhi ya mawaziri waliozungumza na NIPASHE kwa nyakati tofauti
iliyowauliza kama wana watoto wao wanaosoma au waliowahi kusoma katika
shule za kata wamejitetea kuwa wakati shule za Kata zinaanzishwa watoto
wao walikuwa wamemaliza kusoma.
SOPHIA SIMBA
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Sophia Simba,
alisema watoto wake hawakuwahi kusoma katika shule za kata kwa sababu
wakati wanaanza kusoma hazikuwapo.
Hata hivyo, Simba alisema anao wajukuu zake ambao wanasoma katika
shule za kata na kwamba wanakumbana na kero kadhaa ikiwamo kutofundishwa
na walimu.
“Kimsingi watoto wangu hawajasoma katika shule za kata, lakini
ninao wajukuu zangu wanaosoma shule za kata, wanapata matatizo kweli,
walimu hawafundishi,” alisema Simba.
STEVEN WASIRA
Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya rais Mahusiano na Uratibu, Stephen
Wasira, alisema watoto wake wamesoma katika shule za sekondari za
Kilakala, Tanga Ufundi na Forodhani.
Wasira alisema: “Suala la matokeo mabaya ya mtihani wa kidato cha
nne hakuna haja ya kutafuta mchawi, kinachotakiwa ni kuangalia ni namna
gani tutaweza kuboresha elimu yetu nchini.”
“Mimi naungana na hatua ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kuunda tume,
tume hii itatusaidia kujua mapungufu ni nini na namna ya kuyarekebisha,
lakini tukianza kusema watoto wa mtu hawasomi katika shule za kata
haitusaidii,” alisema Wasira.
Wasira aliongeza kuwa hata baadhi ya wafanyabiashara na wanasiasa
watoto wao wengi hawasomi katika shule za kata, lakini hiyo haimaanishi
kuwa shule za kata siyo bora.
HAWA GHASIA
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za
Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia, alisema ana mtoto mmoja ambaye anasoma
katika shule ya sekondari ya Mwanga ambayo inamilikiwa na Jumuiya ya
Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Kwa upande wake, Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe,
alipoulizwa kama ana watoto wanaosoma katika shule za kata alijibu kwa
kifupi kuwa hawezi kujibu swali hilo kwa njia ya simu hadi afuatwe
ofisini.
WILLIAM LUKUVI
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge),
William Lukuvi, alisema suala la kama mawaziri wana watoto wao wanaosoma
shule za sekondari za kata aulizwe Waziri wa Elimu na Mafunzo ya
Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa.
“Mimi ni Coordinator (mratibu) wa serikali siwezi kuzungumzia suala
la kama mawaziri wana watoto wao wanaosoma shule za kata muulize Waziri
wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi,” alisema Lukuvi.
DK. ABDALLAH KIGODA
Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Abdallah Kigoda, alipoulizwa
kama ana watoto wake wanaosoma shule za kata au walisoma katika shule
hizo alisema watoto wake wote ni wakubwa walishamaliza kusoma zamani.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Gerson Lwenge, alisema ana watoto wawili
ambao walisoma shule ya sekondari ya Igwachanya ambayo ni ya kata na
kwamba hivi sasa wanasoma chuo kikuu.
Lwenge alisema baadhi ya shule walimu hawafundishi. Alisema tatizo
lingine ni kwamba wanafunzi hivi sasa wanasomea mitihani na walimu
wanawafundisha kwa ajili ya mtihani tu.
“Kimsingi tatizo la matokeo mabaya pamoja na mambo mengine
linachangiwa na wanafunzi wenyewe kusoma kwa ajili ya mtihani tu
wanakuwa na mitihani ya nyuma, pia walimu hawafundishi na wanafunzi
wanatumia jitihada zao kujisomea,” alisema Lwenge.
SOSPETER MUHONGO
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, alisema kwa
umri alionao hawezi kuwa na mtoto anayesoma katika shule za kata.
“Mimi nipo Uingereza, unaniuliza masuala ya elimu wakati ya kwangu
tu yananitosha, kwanza umri wangu sina mtoto anayesoma shule za kata,”
alisema Profesa Muhongo.
PROFESA MARK MWANDOSYA
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Kazi maalum), Profesa Mark Mwandosya, alisema kwa sasa hana mtoto anayesoma sekondari.
Profesa Mwandosya ambaye alikuwa akizungumza na NIPASHE akiwa nje
ya nchi alisema suala la kuzorota kwa elimu lisichukuliwe kisiasa,
kinachotakiwa ni kujipanga upya kutafuta mbinu za kuboresha elimu
nchini.
“Tukianza kutafuta mchawi tutaanza kurudi nyuma, hii ni karne ya
sayansi na teknolojia, tunatakiwa tujipange ili ifikapo 2025 nchi yetu
iwe ya watu wenye uelewa mzuri na kujiamini,” alisema Profesa Mwandosya.
Profesa Mwandosya alisema changamoto kubwa iliyopo ni kuboresha
shule za sekondari zilizopo badala ya kuanza kuulizana mtoto wa fulani
anasoma katika shule gani jambo ambalo halitasaidia.
CELINA KOMBANI
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma,
Celina Kombani, alisema ana watoto wanne, ambao hakuna hata mmoja
aliyesoma nje ya nchi.
Alisema mwanaye wa kwanza, ambaye hakumtaja jina, alisoma hadi
kidato cha nne katika Shule ya Sekondari Pugu, iliyoko jijini Dar es
Salaam.
Waziri Kombani alisema baadaye mwanaye huyo alisoma Shule ya Alfa
(Father Pekupeku) kidato cha tano na sita, iliyoko mkoani Morogoro na
kwamba, elimu ya juu alisoma katika Chuo Kikuu Mzumbe, kilichopo mkoani
humo.
Alisema mwanaye wa pili, ambaye pia hakumtaja jina, alisoma
sekondari ya Kizuka, iliyoko mkoani humo na kwamba, elimu ya juu alisoma
katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE).
Waziri Kombani alisema mwanaye wa tatu, ambaye vilevile hakumtaja
jina, alisoma kidato cha kwanza hadi sita katika Shule ya Sekondari
Morogoro, wakati Shahada ya Kwanza aliipata katika Chuo Kikuu cha
Tumaini na Shahada ya Pili aliipata Chuo Kikuu Mzumbe.
Alisema mwanaye wa nne, ambaye pia hakumtaja jina, hivi sasa yuko mwaka wa kwanza katika Chuo Kikuu Mzumbe.
“Hakuna mtoto wangu aliyesoma nje. Wakitaka wafanye uchunguzi,” alisema Kombani.
Alisema tatizo la kufaulu na kufeli, liko kwa mtoto mwenyewe na
siyo shule anayosoma, licha ya shule za hapa nchini kukabiliwa na tatizo
la vitendea kazi, ambavyo alisema serikali imekuwa ikilishughulikia.
GAUDENSIA KABAKA
Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka alisema watoto wote ambao
hakutaja idadi yao, akiwamo wa mwisho, ambaye kwa sasa ni marehemu,
walisoma katika shule za kawaida hapa nchini.
Alisema mwanaye wa kwanza, ambaye hakumtaja jina elimu ya msingi
alisoma katika Shule Msingi Bunge, iliyoko jijini Dar es Salaam na
kwamba, walipohamia mkoani Mwanza, aliendelea na elimu hiyo katika Shule
ya Msingi Nyanza.
Alisema mwanaye huyo alisoma hadi kidato cha sita katika Shule ya
Sekondari Wasichana, iliyoko mkoani Tabora na baadaye alisoma elimu ya
juu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).
Hata hivyo, Waziri Kabaka alisema hakubaliani na dhana iliyotawala
vichwani mwa watu wengi kwamba, wazazi wanaowapeleka watoto wao kusoma
kwenye shule za binafsi, ni watu wenye uwezo pekee kifedha.
Alisema hata wazazi wasiokuwa na uwezo nao pia huwapeleka watoto wao kwenda kusoma kwenye shule hizo kwa kujibana kimatumizi.
“Huo utafiti mnaoufanya hautasaidia. Wazazi wanaowapeleka watoto
wao (kusoma) private schools (shule za watu binafsi) siyo wenye hela tu,
hata wasiokuwa na hela pia wanawapeleka,” alisema Waziri Kabaka.
BENEDICT NANGORO
Naibu Waziri wa Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, Benedict Ole Nangoro, alisema hana watoto wanaosoma nje ya nchi.
“Hakuna mtoto wangu hata mmoja anayesoma nje ya nchi, wote wanasoma
hapa nchini tena katika shule za serikali mkoani Arusha,” alisema
Nangoro.
JENISTA MUHAGAMA
Mwenyekiti wa Bunge na Mbunge wa Jimbo la Peramiho (CCM), Jenista
Muhagama, alisema watoto wake wote wanasoma katika vyuo na shule
zilizopo hapa nchini.
Alisema mmoja wa watoto wake amemaliza shule ya Sekondari Matogoro iliyoko Songea na hivi sasa ni mwalimu.
Alisema katika shule hiyo pia wapo watoto wake wawili wanaoendelea na masomo ambao bado hawajamaliza.
SUZAN LYIMO
Waziri kivuli wa Elimu na Mbunge Viti Maalumu (Chadema), Suzan
Lyimo, alisema watoto wake wote wanasoma katika shule za hapa nchini,
mmoja anasoma shule ya Sekondari Ilboru iliyopo jijini Arusha.
Alisema wengine wawili wanasoma katika shule ya msingi Mlimani
iliyopo jijini Dar es Salaam, na mwingine anasoma katika Chuo Kikuu cha
Sayansi na Tiba Muhimbili (Muhas).
MAGDALENA SAKAYA
Mbunge wa Viti Maalumu mkoa wa Tabora (CUF), Magdalena Sakaya,
alisema hana mtoto yeyote anayesoma katika shule za gharama kubwa bali
ana mtoto mdogo wa miaka mitano anayesoma katika shule ya misheni.
KASIMU MAJALIWA
Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi
–Elimu), Kasimu Majaliwa, alisema hana imani kwamba elimu imezorota kwa
sababu watoto wa viongozi wanasoma nje ya nchi na badala yake matokeo
mabaya ya kidato cha nne yamesababishwa na mambo mengi.
“Sisi tumepewa dhamana, tutahakikisha tunatekeleza kikamilifu
kusimamia majukumu yetu. ziko sababu nyingi za watoto kutofanya vizuri,
wapo ambao wamefeli kwa kutosoma kikamilifu, wapo waliokosa vifaa,
walimu au miundombinu mibovu; siyo sababu moja tu ya kusomesha watoto
nje ya nchi,” alisema.
Alisema hakuna Waziri au Mtendaji Mkuu wa Wizara ambaye anakwenda
kazini na kuishia tu kusoma magazeti kwa sababu mtoto wake anakuwa
anasoma nje ya nchi.
“Tuko makini kuona elimu inapata mafanikio, ndiyo maana utaona
serikali inaimarisha miundombinu, inaweka vifaa vya kufundishia na
kujifunzia na kuzalisha walimu wengi kila mwaka.”
Alisema pamoja na mambo mengine, tume iliyoundwa na Waziri Mkuu
itaangalia mitihani iliyopita ilivyotungwa hadi usahihishaji ili kuona
kasoro na kutoa mapendekezo ya nini kifanyike.
Alisema ana watoto wawili na mmoja anasoma Ruangwa wakati mwingine bado hajaanza shule.
Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Amos Makalla,
alisema matokeo mabaya ya wanafunzi katika mtihani huo yametokana na
sababu nyingi zikiwamo za wanafunzi, wazazi na serikali kwa upande
mwingine.
Alisema suala la kusingizia viongozi wa serikali kuwa ndiyo sababu
ya kufeli kwa wanafunzi kwa kuwa hawasomeshi watoto wao kwenye shule za
kata, siyo la kweli kwa kuwa wapo baadhi ya viongozi akiwamo yeye ambaye
wadogo zake wawili aliowasomesha, wamemaliza katika shule za sekondari
za kata huko Mtibwa.
“Kwanza ukisema viongozi wa serikali unakuwa unabagua kwa sababu
utakuwa unaongelea mawaziri, makatibu wakuu na ukaacha wengine kama
wabunge na wafanyakazi wengine serikalini. La msingi hapa ni kuona
tulipokosea na kuparekebisha,” alisema.
Alisema suala la kufeli kwa wanafunzi linatokana na mazingira ya
baadhi ya shule zenyewe kama miundombinu inayohitajika, wanafunzi na
wazazi kwa upande mwingine.
Alisema kwa mfano mwanaye aliyemaliza mwaka jana na ambaye amepata
daraja la nne, hakusoma katika shule za kata kwa sababu hakuchaguliwa
baada ya kumaliza darasa la saba, na badala yake alimpeleka kwenye shule
iliyokuwa na kila kitu; walimu, maabara na maktaba lakini bado alipata
daraja la nne.
Alisema wanafunzi wengi wamefeli kutokana na kutojibidiisha katika
masomo na badala yake wakatumia muda mwingi kwenye ‘facebook’ wakichati
usiku kucha badala ya kusoma.
“Hapa unajiuliza mtoto huyu amepata wapi simu, moja kwa moja
amepewa na mzazi wake. Kwa hiyo nasema, ni vizuri tukaboresha mazingira
ya shule, tukawapa maslahi mazuri walimu, tukaweka maabara, maktaba,
tukaboresha mitaala yetu, lakini pia tukawasimamia watoto wasome, kwa
kuwa unaweza ukampeleka ng’ombe mtoni, lakini huwezi ukamlazimisha
kunywa maji,” alisema.
Wakati mawaziri na baadhi ya wabunge wakieleza hivyo, tayari Waziri
Mkuu Mizengo Pinda ameunda tume maalum itakayofanya uchunguzi wa
matokeo ya mtihani wa kidato cha nne ambayo yalitangazwa na Waziri wa
Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa Februari 18, mwaka huu.
Katika matokeo hayo, asilimia 60 ya wanafunzi waliofanya mtihani wa
kidato cha nne Oktoba, 2012 walifeli kwa kupata daraja sifuri.
Juzi Pinda alitangaza majina ya wajumbe tume hiyo ambao ni
Mwenyekiti wa Tume ni Profesa Sifuni Mchome kutoka tume ya vyuo vikuu,
Makamu mwenyekiti wa tume hiyo ni mbunge wa Viti Maalumu (CCM),
Bernadeta Mshashu.
Wajumbe wa tume hiyo ni pamoja na Mbunge wa Kuteuliwa na Rais,
James Mbatia (NCCR Mageuzi), mbunge wa Kibiti (CCM), Abdul Marombwa,
Profesa Mwajabu Possi (Profesa Mshiriki wa Elimu toka Chuo Kikuu cha Dar
es Salaam), Honoratha Chitanda (Makamu wa Rais Chama cha Waalimu –
CWT), Daina Matemu (Katibu wa Tahossa), Juma Mringo (Mwenyekiti
Tamongsco).

Comments
Post a Comment