Wabunge wamembebesha RC Arusha zigo

Mkuu wa mkoa wa Arusha Magesa Mulongo.
Wabunge wa vyama vya upinzani wa Mkoa wa Arusha wamemtupia lawama Mkuu wa mkoa huo, Magesa Mulongo, kwamba amekuwa akiwatenga kwa kutowashirikisha katika matukio muhimu ya kitaifa yanayofanyika mkoani humo.
 
Wabunge hao wanadai kuwa miongoni mwa shughuli ambazo Mulongo anawatenga zinahusisha ziara za viongozi wa kitaifa na wa kimataifa.
 
Kwa nyakati tofauti wabunge hao walisema Mulongo amekuwa kikwazo katika mkoa huo kwani tangu alipoteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha amekuwa akiwashirikisha wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) peke yao katika matukio mbalimbali yanayofanyika mkoani humo huku akiwatenga wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
 
Wabunge hao wa Chadema walitoa mfano wa ziara ya wiki iliyopita ya Waziri Mkuu wa Denmark, Helle Schimidt, aliyoifanya katika wilaya za Arumeru, Arusha Mjini na Monduli kuwa hawakujulisha ujio wa kiongozi huyo licha ya kwamba wao ni wawakilishi halali wa wananchi katika majimbo hayo.
 
“Mimi nilishasahau kabisa mialiko kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha kunapokuwa na ziara kama Rais, Waziri Mkuu au kiongozi yeyote kutoka nje, huwa naishia kusikia ving’ora kama wananchi wengine na baada ya kuulizia ndipo naelezwa kuwa kuna kiongozi fulani wa kitaifa,” alisema Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema.
 
Lema alisema kuwa Isdory Shirima alipokuwa Mkuu wa mkoa huo, wabunge wa vyama vya upinzani walikuwa wakipata ushirikiano wa kutoka ofisi ya mkuu wa mkoa, lakini tangu ateuliwe Mulongo kushika wadhifa huo, hawashirikishi kabisa.
 
“Ujio wa Waziri Mkuu wa Denmark nilikuwa sifahamu, lakini siku hiyo wakati amefika Arusha nilimpigia simu Mkuu wa Mkoa wa Arusha kumuomba ‘appointment’ (miadi) ya kuonana naye tujadiliane suala la kufungwa kwa barabara ya Kanisa ambayo imekuwa ikilalamikiwa na wananchi ndipo akanieleza niende uwanja wa ndege nikaonane naye huko kwa sababu alikuwa anamsubiri Waziri Mkuu wa Denmark,” alisema Lema.
 
Waziri Mkuu wa Denmark katika ziara yake mjini Arusha, alitembelea Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR) na Makao Makuu ya Ofisi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
 
Akiwa katika Jimbo la Arumeru Mashariki, alitembelea Chuo cha Mafunzo ya Maendeleo na Ushirikiano wa Kimataifa (TCDC) na wakati wa ziara ya Jimbo la Monduli alitembelea Boma la kimasai lililoko katika kijiji cha Nanja.TCDC inaendeshwa kw ushirikiano wa serikali ya Tanzania na Denmark.  
 
Lema alisema siyo kwamba anang’ang’ania kualikwa katika matukio muhimu, lakini serikali ya mkoa wa Arusha lazima itambue kuwa yeye ni mbunge halali ambaye alichaguliwa na maelfu ya wananchi wa Arusha, hivyo ni lazima utaratibu ufuatwe wa kumwalika kama mwakilishi wa wananchi.
 
Naye Mbunge wa Karatu (Chadema), Mchungaji Israel Natse, alisema hawapewi ushirikiano na ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha pamoja na ofisi za wakuu wa wilaya wakati wao ni wawakilishi wa wananchi kwenye majimbo yao.
 
“Ushirikishwaji ni dhaifu sana kwa RC (Mkuu wa Mkoa) na DC (Mkuu wa Wilaya), viongozi wa kitaifa wanapofanya ziara katika majimbo yetu hatujulishwi na tukiuliza tunaambiwa hayo ni mambo ya ‘private’ (binafsi),”alisema Mchungaji Natse.
 
Mchungaji Natse alisema pamoja na mkakati wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya wa kuwatenga katika matukio muhimu, wanashukuru kuwa wananchi katika majimbo yao wanawaamini sana, hivyo mpango huo kama unalenga kutaka kuwadhoofisha kisiasa, kamwe hautafanikiwa. Kwa upande wake Mbunge wa Arumeru Mashariki (Chadema), Joshua Nassari, alisema kama ilivyo kwa wabunge wenzake wa vyama vya upinzania, naye amekuwa akitengwa kwa kutojulishwa na ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha kunapotokea ziara za viongozi wa kitaifa na wa kimataifa.
 
Baadhi ya matukio ambayo wabunge hao walitengwa ni uzinduzi wa jengo la Makao makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Uziduzi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha. Mulongo alipoulizwa na Jamileotz  kuhusiana na  malalamiko ya wabunge hao, alisema amekuwa akiwapatia taarifa za kushiriki katika shughuli mbalimbali kwa kuwapigia simu na siyo kwa kuwaandikia barua kama wanavyotaka. Mulongo alisema kuwa hata hivyo, wabunge hao wa upinzani licha ya kujulishwa, wamekuwa wakitoa udhuru kwamba hawatahudhuria.
 
“Wanang’ang’ania niwaandikie barua, mambo hayo yalishapitwa na wakati, mimi kama Mkuu wa Mkoa ninapokupigia simu bado tu huamini unataka mpaka nikuandikie barua, mbunge hata akinisema hainipunguzii chochote kwa sababu kwanza kazi yangu siyo kualika wabunge,” alisema Mulongo. Mulongo alisema baadhi ya wabunge wanataka wapewe mialiko kwa barua wakati baadhi yao hawakai hata katika ofisi zao. Hata hivyo, hakuwataka kwa majina.
 
Alisema cha msingi wabunge washirikiane na serikali kusaidia kuleta maendeleo ya wananchi wa Mkoa wa Arusha na siyo kuzua malumbano ambayo hayana faida kwa wananchi

Comments

Popular Posts