Wafanyakazi 50 A TO Z waacha kazi

Wafanyakazi zaidi ya 50 kutoka mkoani Tanga wa kiwanda cha kutengeneza vyandarua cha A TO Z, jijini hapa wameacha kazi kwa madai ya kupunjwa posho zao.
 
Wakizungumza na mwandishi wa blogu hii, wafanyakazi hao ambao ni sehemu ya 250 waliotoka mkoani Tanga na kuajiriwa kwenye kiwanda hicho, walisema wameamua kuacha kazi na kurudi nyumbani kwao baada ya mwajiri wao kuwahadaa kwamba angewalipa mshahara mnono na kuwapatia malazi na chakula bure kitendo ambacho hakikuwa hivyo.
 
Akizungumza kwa niaba ya wenzake, mmoja wa wafanyakazi hao, Raymond Erasto, alisema kilichowafanya waamue kuacha kazi katika kiwanda hiyo ni pamoja na manyanyaso ambayo wamekuwa wakiyapata ikiwemo kupewa chakula kisichofaa ambacho ni ugali na mchuzi wa maharage yenye wadudu.
 
‘’Wakati wanakuja kutuchukua mkoani Tanga walituahidi mshahara mnono wa Sh. 250,000 kwa mwezi, kulala bure, lakini cha ajabu chumba tunacholala watu wanne tunakatwa kila mmoja sh. 30,000 kila mwisho wa mwezi,’’ alisema Erasto.
 
Alisema kilichobainika ni kwamba malipo hayo yalikuwa na makato mengi kiasi cha kujikuta baadhi yao wakiambulia Sh. 30,000 kwa mwezi.
 
Mfanyakazi mwingine Athumani Salimu aliutuhumu uongozi wa kiwanda hicho kwa kushindwa kujali maslahi ya wafanyakazi hao kwani kazi wanayoifanya ni ngumu na haiendani na malipo wanayopewa na kukitaka kiwanda hicho kuwatendea haki wafanyakazi wake kwani ipo hatari ya kukimbiwa na wengine iwapo hawatajirekebisha.
 
Naye Afisa mwajiri wa A TO Z,Godwin Obed akizungumza kwa njia ya simu kutoka mkoani Tanga alikanusha wafanyakazi hao kulipwa Sh 30,000 kwa mwezi na kufafanua kuwa baadhi yao hawaingii kazini na taratibu za kiwanda ni lazima wakatwe sehemu ya malipo yao.
 
Aliongeza kuwa wafanyakazi hao hulipwa vizuri stahili zao kama makubaliano yalivyokuwa, ila kuna makato ya kisheria kama NSSF na mengine ambayo ni lazima yakatwe, hivyo kitendo cha kudai kwamba wanalipwa kidogo na kupewa chakula kibovu hayana ukweli wowote.
 
''Sisi tumechukua wafanyakazi 250 kutoka Tanga kwa hiyo hao 50 unaosema wameachakazi hawatusumbui wao waende watakuja wengine,''alisema Obed kwa njia ya simu.
 
Kiwanda hicho chenye wafanyakazi zaidi ya 3000 kimekuwa na msuguano wa mara kwa mara na wafanyakazi hao kiasi cha kuulazimu uongozi wa kiwanda hicho kubuni mkakati wa kuajiri wafanyakazi kutoka mikoa tofauti hapa nchini baada ya wengi wao kushindwa kufanya kazi na kuacha kwa madai ya malipo kidogo

Comments

Popular Posts